Tanzania
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania | |
|---|---|
| Kaulimbiu: "Uhuru na Umoja" | |
| Wimbo wa taifa: "Mungu ibariki Afrika" | |
| Mji mkuu | Dodoma |
| Mji mkubwa | Dar es Salaam |
| Lugha rasmi | |
| Lugha ya taifa | Kiswahili |
| Kabila | Kupita makabila 125 |
| Dini | 63.1% Wakristo 34.1% Waislamu 1.50% Wasio na dini 1.20% Dini asilia 0.1% wengine |
| Uraia | Mtanzania |
| Serikali | Jamhuri |
| Samia Suluhu Hassan | |
| Deogratius Ndejembi | |
| Mwigulu Nchemba | |
| Tulia Ackson | |
• Jaji Mkuu | George Mcheche Masaju |
Uhuru kutoka Ufalme wa Muungano | |
| 9 Desemba 1961 | |
| 10 Desemba 1963 | |
• Muungano | 26 Aprili 1964 |
• Katiba ya sasa | 25 Aprili 1977 |
| Eneo | |
| • Jumla | km2 947 303[1] |
| • Maji (asilimia) | 6.4[1] |
| Idadi ya watu | |
| • Kadirio la 2023 | 65 642 682[1] |
| • Sensa ya 2022 | 61 741 120[2] |
| PLT (PPP) | Kadirio la 2025 |
| • Jumla | |
| • Kwa kila mtu | |
| PLT (Kawaida) | Kadirio la 2025 |
| • Jumla | |
| • Kwa kila mtu | |
| HDI (2022) | kati |
| Sarafu | Shilingi ya Tanzania |
| Majira ya saa | UTC+3 (Afrika Mashariki) |
| Muundo wa tarehe | siku/mwezi/mwaka |
| Upande wa magari | Kushoto |
| Msimbo wa simu | +255 |
| Msimbo wa ISO 3166 | TZ |
| Jina la kikoa | .tz |
Tanzania, rasmi Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, ni nchi iliyoko Afrika Mashariki ndani ya eneo la Maziwa Makuu ya Afrika na kando ya pwani ya Bahari ya Hindi. [5] Inapakana na Kenya na Uganda kaskazini, Rwanda, Burundi, na Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo magharibi, na Zambia, Malawi, na Msumbiji kusini. [6] Kufikia mwaka 2024, inakadiriwa kuwa na idadi ya watu takriban milioni 67 [2]. , ikiwa nchi ya 20 duniani na ya 5 Afrika kwa idadi ya watu. Mji mkuu ni Dodoma, huku Dar es Salaam ukiwa mji wake mkubwa na kituo kikuu cha kiuchumi. [6] Nchi hii imegawanywa katika mikoa 31 ya kiutawala, na lugha rasmi ni Kiswahili na Kiingereza. [5]
Mabaki mengi muhimu ya zamadamu yaligunduliwa nchini Tanzania.[5] Katika zama za Mawe na Shaba, kulikuwa na uhamaji wa kihistoria kutoka kaskazini kuingia Tanzania wa wazungumzaji wa Kikushi cha Kusini waliokuwa na sifa kama za Wairaqw wa leo, waliotoka Ethiopia ya leo; pia kulikuwepo na watu wa Kikushi cha Mashariki waliotoka kaskazini mwa Ziwa Turkana kati ya miaka 2,000 hadi 4,000 iliyopita; pamoja na Waniloti wa Kusini kama Wadatooga, waliotokea katika mpaka wa Sudan Kusini na Ethiopia takribani miaka 2,900 hadi 2,400 iliyopita. Uhamiaji huo ulifanana kwa wakati na ujio wa Wabantu wa Mashariki kutoka Afrika Magharibi waliotua katika maeneo ya Ziwa Viktoria na Ziwa Tanganyika.[7]
Katika karne ya 19, Tanzania bara ilikuwa chini ya utawala wa Wajerumani kama sehemu ya Afrika ya Mashariki ya Kijerumani, na baada ya Vita Kuu ya Kwanza ya Dunia, Waingereza walichukua mamlaka kwa jina la Tanganyika, huku Visiwa vya Zanzibar vikisalia katika usimamizi tofauti wa kikoloni.[8] Baada ya kupata uhuru mwaka 1961 (Tanganyika) na 1963 (Zanzibar), nchi hizo mbili ziliungana mwaka 1964 na kuunda Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Tanganyika iliingia katika Jumuiya ya Madola na Tanzania kwa sasa ni mwanachama wa jumuiya hiyo kama taifa moja.[9]
Leo, kikatiba Tanzania ni jamhuri ya urais inayofuata mfumo wa vyama vingi lakini imekuwa chini ya chama kimoja kikuu ambacho kimeshikilia madaraka moja kwa moja tangu uhuru ingawa jina lake lilibadilika kutoka Tanganyika African National Union hadi Chama cha Mapinduzi mwaka 1977.[10] Tanzania haijawahi kupitia machafuko makubwa ya ndani tangu uhuru, na inahesabiwa kuwa miongoni mwa nchi salama na tulivu zaidi kisiasa barani Afrika.[8]
Idadi ya watu wa Tanzania inajumuisha makabila, lugha, na dini zaidi ya 120. Ukristo ndio dini yenye wafuasi wengi, ikifuatwa na Uislamu na dini za jadi.[11] Tanzania ndiyo nchi yenye tofauti kubwa zaidi za lugha Afrika ya Mashariki. Ingawa hakuna lugha rasmi kisheria, Kiswahili hutumika kama lugha ya taifa, na Kiingereza hutumika katika biashara za kimataifa, diplomasia, mahakama za juu, na elimu ya sekondari na ya juu. Kiarabu huzungumzwa pia visiwani Zanzibar.[5]
Kijiografia, Tanzania ina milima na misitu mingi kaskazini-mashariki, ikiwemo Mlima Kilimanjaro, mlima mrefu zaidi Afrika na mlima pekee wa kujitegemea kwa kimo duniani.[12] Maziwa Makuu ya Afrika yote matatu yanapatikana kwa sehemu ndani ya Tanzania: Ziwa Viktoria (ziwa kubwa zaidi Afrika), Ziwa Tanganyika (ziwa lenye kina kirefu zaidi na samaki wa pekee), na Ziwa Nyasa upande wa kusini. Ukanda wa pwani una joto na unyevunyevu, na Visiwa vya Zanzibar vipo karibu na mwambao. Eneo la Hifadhi ya Menai Bay ni eneo kubwa zaidi la hifadhi ya baharini Zanzibar. Maporomoko ya Kalambo yaliyoko mpakani na Zambia ndiyo maporomoko ya pili kwa urefu barani Afrika. Tanzania ni moja ya nchi maarufu duniani kwa safari za utalii.[13]
Jina
Jina "Tanzania" liliundwa kama mkusanyiko wa majina ya maeneo mawili yaliyoungana kuunda nchi: Tanganyika na Zanzibar.[14] Jina lilipatikana kwa mashindano yaliyotangazwa mwaka 1964 na serikali kutafuta jina fupi zaidi kuliko "Jamhuri ya Tanganyika na Zanzibar".
Mshindi alikuwa mwenyeji wa Dar es Salaam aliyeitwa Mohamed Iqbal Dar (1944 - 2025) [15]. Alipendekeza kuunganisha herufi tatu za kwanza za TANganyika na ZANzibar akafikia "Tanzan". Hakuridhika bado, akaona nchi nyingi za Afrika zina majina yanayoishia na "ia" akaongeza herufi hizi. Mwenyewe alieleza baadaye chaguo lake kwamba aliamua kutumia "I" ya jina lake Iqbal na "A" ya jina la madhehebu yake aliyoyafuata katika Uislamu ya Ahmadiyya.[16]
Jina "Tanganyika" linatokana na maneno ya Kiswahili "tanga" na "nyika", yakiunda msemo "tanga nyikani". Wakati fulani inaelezwa kama marejeleo ya Ziwa Tanganyika. [17] Jina la Zanzibar linatokana na "zenji", jina la watu wa eneo hilo (inadaiwa lina maana ya "nyeusi"), na neno la Kiarabu "barr", ambalo linamaanisha pwani au ufukwe.[18]
Historia

Historia ya Tanzania inawakilisha historia ya eneo ambalo leo linaunda Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, ikijumuisha Tanganyika Bara na visiwa vya Zanzibar. Ugunduzi wa akiolojia katika Bonde la Oltupai na maeneo mengine unaonyesha kuwa eneo hili limekuwa na makazi ya binadamu tangu nyakati za kale sana na lina baadhi ya ushahidi muhimu zaidi kuhusu mageuzi ya awali ya binadamu. [19] Kwa karne nyingi, eneo hili lilikaliwa na jamii mbalimbali, zikiwemo jamii zinazozungumza lugha za Kibantu, huku maeneo ya pwani yakijumuishwa katika mitandao ya biashara ya Bahari ya Hindi iliyounganisha Afrika Mashariki na Uarabuni, Uajemi, Uhindi, na baadaye China. [20]
Kuanzia kipindi cha kati cha historia, miji kadhaa ya Waswahili ilistawi kando ya pwani, ikiwemo Kilwa, ambayo ilikuja kuwa kitovu muhimu cha biashara na utamaduni. [21] Ushawishi wa Wareno ulijitokeza katika sehemu za pwani katika karne ya 16, lakini baadaye ukachukuliwa na Waarabu wa Omani, hasa Zanzibar. Katika karne ya 19, Zanzibar iliibuka kama kituo muhimu cha biashara, huku upanuzi wa ukoloni wa Ulaya ukiongezeka katika maeneo ya bara. Kufikia mwishoni mwa karne ya 19, sehemu kubwa ya Tanzania Bara ilikuwa imekuwa sehemu ya Afrika ya Mashariki ya Kijerumani. [22]
Baada ya Ujerumani kushindwa katika Vita vya Kwanza vya Dunia, Tanganyika iliwekwa chini ya utawala wa Uingereza kama eneo la mamlaka ya Ligi ya Mataifa na baadaye eneo la udhamini la Umoja wa Mataifa. Harakati za uzalendo ziliongezeka baada ya Vita vya Pili vya Dunia, zikiongozwa hasa na Julius Nyerere na Chama cha Tanganyika African National Union (TANU). [23] Tanganyika ilipata uhuru kutoka kwa Uingereza tarehe 9 Desemba 1961 na kuwa jamhuri mwaka 1962, huku Nyerere akiwa rais wake wa kwanza. [24]
Zanzibar, mapinduzi yaliyotokea Januari 1964 yaliuangusha utawala wa Kisultani uliotawaliwa na Waarabu na kusababisha kuundwa kwa serikali mpya. [25] Baadaye mwaka huo, Tanganyika na Zanzibar ziliungana na kuunda Jamhuri ya Muungano wa Tanzania tarehe 26 Aprili 1964. Chini ya uongozi wa Nyerere, Tanzania ilifuata sera za ujamaa wa Kiafrika zilizojulikana kama Ujamaa, kabla ya mageuzi ya kiuchumi na kufunguliwa kwa mfumo wa kisiasa kuanzishwa mwishoni mwa karne ya 20. [26] Tangu wakati huo, Tanzania imeendelea kuwa jamhuri huru na mwanachama muhimu wa mashirika ya kikanda kama Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC) na Umoja wa Afrika (AU). [6]
Jiografia
Ikiwa na eneo la kilomita za mraba 947,303 (365,756 sq mi), Tanzania ni nchi ya 13 kwa ukubwa barani Afrika na ya 31 kwa ukubwa duniani.[27] Inapakana na Kenya na Uganda upande wa kaskazini; Rwanda, Burundi, na Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo upande wa magharibi; na Zambia, Malawi, na Msumbiji upande wa kusini.

Tanzania iko kwenye pwani ya mashariki ya Afrika na ina ufuo wa Bahari ya Hindi takriban kilomita 424 (885 mi).[28] Pia inajumuisha visiwa kadhaa vya pwani, vikiwemo Unguja (Zanzibar), Pemba, na Mafia. Tanzania ni nchi yenye sehemu za juu na za chini kabisa barani Afrika: Mlima Kilimanjaro, wenye urefu wa mita 5,895 (futi 19,341) juu ya usawa wa bahari, na kina cha Ziwa Tanganyika, katika mita 1,471 (futi 4,826) chini ya usawa wa bahari kwa mtiririko huo.

Tanzania ina milima na misitu minene kaskazini-mashariki, ambako kuna Mlima Kilimanjaro. Nchi iko katika eneo la Maziwa makubwa ya Afrika, hivyo maziwa yanafunika km2 61,500, yaani 6% za eneo lote la nchi. Upande wa kaskazini na magharibi kuna Ziwa Victoria, ziwa kubwa zaidi barani Afrika, na Ziwa Tanganyika, ziwa lenye kina kirefu zaidi barani humo, linalojulikana kwa aina yake ya kipekee ya samaki. Upande wa kusini magharibi kuna Ziwa Nyasa. Eneo la katikati mwa Tanzania ni uwanda mkubwa, wenye tambarare na ardhi ya kilimo. Ukanda wa mashariki una joto na unyevunyevu, huku Visiwa vya Zanzibar vikiwa karibu. Maporomoko ya maji ya Kalambo katika mkoa wa kusini-magharibi mwa Rukwa ni maporomoko ya pili kwa urefu barani Afrika, na yanapatikana karibu na ufuo wa kusini-mashariki wa Ziwa Tanganyika kwenye mpaka na Zambia. [29] Eneo la Hifadhi ya Menai Bay visiwani Zanzibar ndilo eneo kubwa zaidi la bahari lililohifadhiwa.
Hali ya hewa

Hali ya hewa inatofautiana sana ndani ya Tanzania. Katika nyanda za juu, halijoto huanzia 10 hadi 20 °C (50 na 68 °F) wakati wa msimu wa baridi na joto kwa mtiririko huo.
Tanzania hupata majira ya joto katika miezi ya Desemba, Januari na Februari (25–31 °C au 77.0–87.8 °F) huku kipindi cha baridi zaidi kikitokea kati ya Mei na Agosti (15–20 °C au 59–68 °F). Halijoto ya kila mwaka ni 20 °C (68.0 °F).
Hali ya hewa ni baridi katika maeneo ya milima mirefu. Tanzania ina vipindi viwili vikuu vya mvua: mvua za vuli hunyesha katika miezi ya Oktoba, Novemba na Desemba na mvua za masika hunyesha katika miezi ya Machi, Aprili na Mei ingawa zipo tofauti ndogo kati ya sehemu mbalimbali.[30] Kiasi cha mvua na halijoto husababisha tofauti za aina ya uoto wa asili, udongo na aina ya mazao yanayolimwa.
Mabadiliko ya hali ya hewa nchini Tanzania yanasababisha kuongezeka kwa joto na uwezekano mkubwa wa matukio ya mvua kubwa (kusababisha mafuriko) na vipindi vya ukame.[31][32] Mabadiliko ya hali ya hewa tayari yanaathiri sekta za kilimo, rasilimali za maji, afya na nishati nchini Tanzania. Kupanda kwa kina cha bahari na mabadiliko ya ubora wa maji kunatarajiwa kuathiri uvuvi na ufugaji wa samaki.[33]

Tanzania ilitoa Mpango wa Kitaifa wa Kukabiliana na Mabadiliko ya Tabianchi (NAPAs) mwaka 2007 kama ilivyoagizwa na Mkataba wa Umoja wa Mataifa wa Mabadiliko ya Tabianchi. Mwaka 2012, Tanzania ilitoa Mkakati wa Kitaifa wa Mabadiliko ya Tabianchi ili kukabiliana na wasiwasi unaoongezeka wa athari mbaya za mabadiliko ya tabianchi katika mazingira ya kijamii na kiuchumi.[34]
Wanyamapori na Hifadhi
Tanzania ina takriban 20% ya spishi za wanyama wengi wa Afrika wenye damu moto, wanapatikana kwenye mbuga zake za Taifa, hifadhi na bahari. Hifadhi za Taifa na mbuga za wanyama zimeenea katika eneo la zaidi ya kilomita za mraba 42,000 (sq. mi 16,000) na kuunda karibu 38% ya eneo la nchi.[35][36] Tanzania ina mbuga 21 za taifa, pamoja na hifadhi mbalimbali za wanyamapori na misitu, ikijumuisha Hifadhi ya Ngorongoro. Magharibi mwa Tanzania, Hifadhi ya Taifa ya Gombe ni kitovu ya uchunguzi unaoendelea wa Jane Goodall wa tabia ya sokwe, ambao ulianza mwaka wa 1960.[37][38]
Tanzania ina bioanuwai nyingi na ina aina mbalimbali za makazi ya wanyama.[39] Katika uwanda wa Serengeti nchini Tanzania, nyumbu (Connochaetes taurinus mearnsi), "bovids" wengine na pundamilia[40] hushiriki katika uhamaji mkubwa wa kila mwaka. Tanzania ni nyumbani kwa takriban spishi 130 za amfibia na zaidi ya spishi 275 za wanyama watambaao, wengi wao wanapatikana Tanzania tu na wamejumuishwa katika orodha ya International Union for Conservation of Nature.[41] Tanzania ina idadi kubwa ya simba duniani.[42]
Tanzania ilikuwa na alama 7.13/10 kwenye Forest Landscape Integrity Index mwaka 2019, ilishika nafasi ya 54 duniani kati ya nchi 172.[43]
Serikali na Utawala
Muundo wa uongozi na utawala katika kipindi cha ukoloni ulizingatia mgawanyo wa madaraka baina ya mihimili mitatu ya dola yaani serikali, bunge na mahakama.
Tangu uhuru, mgawanyo wa madaraka na uhusiano miongoni mwa mihimili hiyo uliimarishwa kwa kuzingatia wakati, mahitaji ya demokrasia na misingi ya utawala bora na umeainishwa pia katika katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Ibara ya 4 (1).
Kuwepo kwa mfumo wa vyama vingi pia kulikuwa hatua ya kuendelea kuimarisha utawala wa ushiriki wa wananchi kadiri mahitaji ya upanuzi wa maono na falsafa duniani.
Ugatuzi, yaani mgawanyo wa kiutawala, unafuata Katiba ya nchi I 2.2. Tanzania imegawiwa kwa mikoa 31. Kila mkoa huwa na wilaya ndani yake. Jumla ya wilaya ni 169, ambazo kati yake 34 ni miji.
Ndani ya wilaya kuna ngazi za tarafa na kata.
Chini ya kata kuna vijiji na wakati mwingine ngazi ya chini tena ambayo ni vitongoji.
Miundo ya muungano
Tangu muungano wa Tanganyika na Zanzibar kufanyika mwaka 1964 Tanzania imekuwa na miundo ifuatayo:
- Nchi inatawaliwa na serikali ya muungano ikitekeleza sheria zinazotolewa na bunge la Tanzania.
- Tanganyika au Tanzania bara haina serikali wala bunge la pekee.
- Zanzibar (visiwa vya Unguja na Pemba) ina serikali na bunge lake vinavyoratibu mambo yasiyo ya muungano.
Mambo yafuatayo yamekubalika kuwa shughuli za muungano:
- Mambo ya nje
- Jeshi
- Polisi
- Mamlaka ya dharura
- Uraia
- Uhamiaji
- Biashara ya nje
- Utumishi wa umma
- Kodi ya mapato, forodha
- Bandari, Usafiri wa anga, Posta na Simu
Demografia

Watu wa Tanzania hawaenei sawasawa. Katika maeneo makavu sana, kwa wastani kuna mtu mmoja tu kwa kilomita ya mraba (1/km²), lakini sehemu zenye rutuba za bara, kuna watu 51 kwa kila kilomita ya mraba. Hatimaye huku